* Yapanda miti kutekeleza malekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan kuhusu kutunza mazingira na kutekeleza maendeleo endelevu
* Yatoa faraja kwa Wafungwa gereza la Isanga, Dodoma
MFUKO wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF), unashirikiana na Serikali katika kuboresha maisha ya Watanzania kupitia uhakika wa matibabu kwa utaratibu wa bima ya Afya. Mfuko pia unawajibikaji kwa jamii (corporate Social responsibility).
Katika kuelekea kilele cha Siku ya Wanawake Duniani ambayo huadhimishwa kila mwaka tarehe 8 Machi, NHIF hushiriki maadhimisho hayo kwa kuungana na wanawake wote duniani.
Mwaka huu NHIF inashiriki maadhimisho haya kwa namna ya pekee ambapo imetumia fursa hiyo kutekeleza lengo la maendeleo uendelevu kwa upandaji wa miti mkoani Dodoma ili kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
Februali 28, 2026, Watumishi wa kike wa NHIF walikutana Makao Makuu Dodoma kwa ajili ya kupanda miti katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Dodoma ikiwemo Mji wa Serikali Mtumba, Hospitali ya Uhuru iliyopo Wilaya ya Chamwino na Ofisi za NHIF Makao Makuu.
Mbali na zoezi hilo ambalo lilifanikisha upandaji wa jumla ya miche 500 kwa awamu ya kwanza, Watumishi hao pia walitembelea Gereza la Isanga kwa ajili ya kuonesha matendo ya huruma kwa wafungwa kwa kuwapelekea misaada mbalimbali ikiwemo unga wa lishe, dawa za meno, mafuta ya kupaka na taulo za kina mama, nguo za watoto pamoja na vitabu vya ibada. Watumishi hao walipata fursa ya kuzungumza na wafungwa na kuwa dua ya pamoja.
Akizungumza na Watumishi mapema kabla ya kuanza kwa shughuli hizo, Mkurugenzi Mkuu wa NHIF, Dkt. Irene Isaka alisema kuwa shughuli ya upandaji miti ni muhimu kwa kuwa ni utekelezaji wa Malengo ya maendeleo endelevu na Dira ya Taifa 2025 inayolenga kuhifadhi mazingira, kuboresha vyanzo vya maji, kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na kufikia malengo ya ajenda za kimataifa za mazingira.
“Leo wote kwa umoja wetu kama Watumishi wanawake wa NHIF tutapanda zaidi miche 500 na huu ni mwanzo tu lakini tutakuwa na mazoezi kama haya mara kwa mara ofisi zote nchini ili kila mtumishi aweze kupanda miti mingi zaidi,” alisema Dkt. Isaka.
Alisema kuwa mbali na upandaji miti pia, Mfuko kupitia Kundi la wanawake watashiriki kufanya matendo ya huruma.

Kuelekea siku ya wanawake Duniani wanawafe wa Mfumo wa Taifa wa Bima ya Afya wamefanya matendo ya huruma katika Gereza la isanga ikiwa ni sehemu ya kurejesha kwa jamii.
Alitumia fursa hiyo kuwashukuru Watumishi wote kwa kuendelea kufanya kazi kwa kujituma na kwa weledi katika kuwahudumia wananchi hususan kipindi hiki ambacho usajili wa wananchi wanaotoka Kaya zisizo na uwezo ukiendelea katika mikoa yote kupitia mpango wa Bima ya Afya kwa Wote.
Alitimia fursa hiyo kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan kwa kuhakikisha bima ya afya inamfikia kila mtanzania. Aliushukuru uongozi wa Wizara ya afya kwa ushirikiano Mkubwa hasa kutoka kwa Waziri wa Afya Mh. Mohamed Mchengerwa (MB), Naibu Waziri Dkt Florence Samizi (MB), Katibu Mkuu Dkt Seif Shekalage, Naibu Katibu Mkuu Eng. Ismail Rumatila na Mganga Mkuu wa Serikali Dkt Grace Maghembe.
Bima ya Afya kwa Wote, jiunge sasa